Pages

Friday, 10 February 2012

Shaka


  Alizaliwa 1781 - 1828 alikuwa kiongozi wa Wazulu aliyebadilisha ukoo mdogo wa Kinguni kuwa kabila au taifa kubwa lililotawala maeneo mapana ya Afrika Kusini hasa Natal ya leo.
Sifa zake zimetokana na uwezo wa kupanusha utawala wake kutoka eneo ndogo la 260 km² kuwa 28.500 km², kuvunja nguvu ya makabila mengine na kuyaunganisha na taifa lake. Katika historia ya kijeshi ya Afrika alianzisha mbinu mpya zilizopanusha uwezo na enzi yake. Sifa hizi, jinsi ilivyo mara nyingi na viongozi wanaotegemea nguvu ya kijeshi, zimeenda pamoja na vita na uharibufu mwingi. Miaka ya Shaka ilianzisha kipindi cha mfecane yaani "uharibifu" kinachokumbukwa na mataifa mengi ya Afrika Kusini.


Jina lake linatokana na neno la kizulu "iShaka" linalomaanisha mdudu ambaye katika imani ya utamaduni wa Kizulu anasemekana kuvuruga hedhi ya kinamama. Jina hili ni dalili la kuzaliwa nje ya ndoa. Hivyo miaka ya kwanza ya Shaka ilikuwa miaka migumu bila baba jambo ambalo lilimfanya aone kama anadharauliwa na watu wengine. Utoto huu ulisababisha hasira ndani yake akalipiza kisasi baadaye.

Kama kijana Shaka alikaa kwa kabila kubwa zaidi ya Mthethwa alikoingia pamoja na hirima yake katika jeshi. Wakati ule ukoo wa Wazulu ulikubali Wamthehtwa kuwa mabwana wao. Chifu wa Mthethwa alikuwa Dingiswayo aliyeanzisha utaratibu mpya wa impi yaani kupanga watu wake vitani katika vikundi na kuwa na ngazi mbalimbali za mamlaka. Shaka alihudumia miaka sita katika vita za Dingiswayo akawa hodari sana na kujifunza uongozi alioboresha baadaye.
Baada ya kifo cha babake Shaka alirudi kwa Wazulu kwa msaada wa Dingiswayo akachukua uongozi mnamo mwaka 1812. Baada ya kuwa kiongozi akalipiza kisasi maadui wa utoto wake akiwaua kwa njia mbalimbali.
Shaka aliendelea kukubali ubwana wa Mthethwa na Dingiswayo hadi akauwawa vitani na kabila la Ndwandwe mwaka 1817. Lakini pamoja na hayo alipigana vita na makabila madogo jirani. Mbinu yake ilikuwa kuwashambulia waliompinga au kuwa hatari kwake; wanawake na watoto waliingizwa katika ukoo wake, pamoja na wanajeshi wa kiadui wasiouawa lakini waliokubali kumfuata baada ya kushindwa. Kwa njia hiyo ukoo mdogo wa Wazulu uliendelea kukua.

Katika miaka iliyofuata Shaka aliendelea kushambulia vikundi vya jirani na kuwaingiza katika utawala wake. Makabila mengine walimfuata bila vita wakikubali uongozi wake na kuingiza vijana wao katika impi au vikosi vya kijeshi vya Shaka. Alituma viongozi au majenerali wake pamoja na impi pande mbalimbali hadi Msumbiji au pia Zimbabwe. Vikundi kama Ndebele huko Zimbabwe au hata Wangoni katika Tanzania ni matokeo ya matembezi ya impi za kizulu zilizoenda mbali na kupoteza mawasiliano na nyumbani.
Vita hizi zilisababisha makabila mengine kukimbia na kuhamahama wakishambulia majirani zao hivyo kupanusha eneo la vita katika nchi mbali na Wazulu wenyewe. Kipindi hiki kinakumbukwa kwa majina kama "mfecane" (Kizulu) au "difaqane" (Kisotho) kuwa miaka 30 ya vita na kifo.
Pamoja na hayo makabila mengine kama Wasotho, Waswazi, Wandebele au Wagaza walioshambuliwa walijifunza mbinu za kijeshi wakifaulu kujitetea na kuanzisha mataifa makubwa yakiunganisha wenyewe koo na makabila madogo zaidi.
Utawala wa Shaka ulikuwa na tabia za kinyama zilizosababisha chuki nyingi dhidi yake. Baada ya kifo cha mamake Nandi alikuwa na hasira kiasi cha kuuwa watu 7000 kati ya wanajeshi wake kwa kosa la kutoonyesha huzuni ya kutosha na kuamuru kipindi cha kufunga miezi mitatu. Aliamuru mashamba yasilimwe kwa mwaka mmoja na kila mwanamke aliyeonekana kuwa na mimba katika kipindi hiki aliuawa pamoja na mumewe. Wataalamu wengine huona ya kwamba wakati ule Shaka alionekana kuwa na kichaa. Maadui walifanya mipango dhidi yake mwishowe aliuawa na ndugu zake. Mwaka 1828 impi nyingi zilikuwa mbali vitani ikuli ikawa bila ulinzi wa kutosha. Kaka zake Dingane na Mhlangana walimwua na kutupa maiti shimoni.
Dingane alimfuata Shaka akaua vingozi wengi waliokuwa waaminifu kwa Shaka.
Alilazimisha watu wake kuacha vyandalua na viatu na kutembea pekupeku. Hii iliongeza kasi ya impi zake na uwezo wao wa kushambulia haraka. Inasemekana ya kwamba Shaka aliuwa wote waliolalamika walipoamriwa kuacha viatu vyao.


No comments:

Post a Comment